Biblia ya King James Version

Yohana, Sura ya 17:

  1. Maneno hayo aliyasema Yesu, akainua macho yake mbinguni, akasema, Baba, saa imefika; mtukuze Mwana wako, ili Mwanao naye akutukuze wewe;
  2. kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele.
  3. Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.
  4. Nimekutukuza duniani, nimemaliza kazi uliyonipa niifanye.
  5. Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.
  6. Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu; walikuwa wako, ukanipa mimi; nao wamelishika neno lako.
  7. Sasa wamejua ya kuwa yote uliyonipa yatoka kwako.
  8. Kwa maana maneno uliyonipa nimewapa wao; nao wamezipokea, na wamejua hakika ya kuwa nalitoka kwako, na wamesadiki ya kwamba ndiwe uliyenituma.
  9. Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu, bali wale ulionipa; maana hao ni wako.
  10. Na wote walio wangu ni wako, na wako ni wangu; nami nimetukuzwa ndani yao.
  11. Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. Baba Mtakatifu, walinde kwa jina lako ulilonipa, ili wawe na umoja kama sisi.
  12. Nilipokuwa pamoja nao katika ulimwengu, niliwalinda kwa jina lako ulilonipa; ili andiko litimie.
  13. Na sasa naja kwako; na mambo haya nayasema ulimwenguni, ili wawe na furaha yangu ikamilike ndani yao.
  14. Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia, kwa sababu wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.
  15. Siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu, bali uwalinde na yule mwovu.
  16. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.
  17. Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli.
  18. Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami pia nimewatuma wao ulimwenguni.
  19. Na kwa ajili yao najiweka wakfu mwenyewe, ili wao pia watakaswe katika ukweli.
  20. Wala si hao tu ninaowaombea, bali na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao;
  21. Ili wote wawe kitu kimoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako, hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba ndiwe uliyenituma.
  22. Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja.
  23. Mimi ndani yao, nawe ndani yangu, ili wawe wamekamilika katika umoja; ili ulimwengu ujue ya kuwa wewe ndiwe uliyenituma, na kuwapenda wao kama ulivyonipenda mimi.
  24. Baba, hao ulionipa nataka wawe pamoja nami mahali nilipo; ili wauone utukufu wangu ulionipa, kwa maana ulinipenda kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu.
  25. Baba mwenye haki, ulimwengu haukukujua, lakini mimi nimekujua, na hawa wamejua ya kuwa wewe ndiwe uliyenituma.
  26. Nami naliwajulisha jina lako, nami nitawajulisha hilo, ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami ndani yao.