Biblia ya King James Version

Yohana, Sura ya 15:

  1. Mimi ndimi mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima.
  2. Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa.
  3. Sasa ninyi mmekuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia.
  4. Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; hamwezi tena, msipokaa ndani yangu.
  5. Mimi ni mzabibu, ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote.
  6. Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; na watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea.
  7. Ninyi mkikaa ndani yangu na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa.
  8. Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu.
  9. Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi; kaeni katika pendo langu.
  10. Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake.
  11. Hayo nimewaambia, ili furaha yangu ikae ndani yenu, na furaha yenu ikamilike.
  12. Amri yangu ndiyo hii, Mpendane kama nilivyowapenda ninyi.
  13. Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.
  14. Ninyi ni rafiki zangu mkitenda ninayowaamuru.
  15. Tangu sasa siwaitii watumwa; kwa maana mtumwa hajui afanyalo bwana wake; kwa maana yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewajulisha.
  16. Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda, na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni.
  17. Haya ninayowaamuru ninyi mpendane.
  18. Kama ulimwengu ukiwachukia ninyi, mwajua kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi.
  19. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi niliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia.
  20. Kumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wameniudhi mimi, watawaudhi ninyi pia; ikiwa wamelishika neno langu, watalishika lenu pia.
  21. Lakini haya yote watawatenda ninyi kwa ajili ya jina langu, kwa sababu hawamjui yeye aliyenituma.
  22. Kama nisingalikuja na kusema nao, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa hawana la kujificha kwa dhambi yao.
  23. Anayenichukia mimi humchukia na Baba yangu pia.
  24. Kama nisingalifanya kati yao kazi asizozifanya mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wameniona na kunichukia mimi na Baba yangu pia.
  25. Lakini hii hutukia ili neno lililoandikwa katika torati yao litimie, Walinichukia bila sababu.
  26. Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia.
  27. Na ninyi pia mtashuhudia, kwa sababu mmekuwa pamoja nami tangu mwanzo.