Biblia ya King James Version

Yohana, Sura ya 10:

  1. Amin, amin, nawaambia, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, bali akwea na njia nyingine, huyo ni mwivi na mnyang’anyi.
  2. Bali yeye aingiaye kwa mlango ndiye mchungaji wa kondoo.
  3. Bawabu humfungulia yeye; na kondoo huisikia sauti yake, naye huwaita kondoo wake kwa majina, na kuwaongoza nje.
  4. Naye awatoapo nje kondoo wake mwenyewe, huwatangulia, na kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake.
  5. Wala mgeni hawatamfuata, bali watamkimbia; kwa maana hawaijui sauti ya wageni.
  6. Yesu aliwaambia mfano huo, lakini wao hawakuelewa aliyokuwa akiwaambia.
  7. Basi Yesu akawaambia tena, Amin, amin, nawaambia, Mimi ndimi mlango wa kondoo.
  8. Wote walionitangulia ni wezi na wanyang’anyi, lakini kondoo hawakuwasikia.
  9. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka, ataingia na kutoka, na kupata malisho.
  10. Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.
  11. Mimi ndimi mchungaji mwema: mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.
  12. Lakini mtu wa mshahara, wala si mchungaji, ambaye kondoo si mali yake, humwona mbwa-mwitu anakuja, akawaacha kondoo na kukimbia, na mbwa-mwitu huwakamata na kuwatawanya.
  13. Mtu wa mshahara hukimbia kwa sababu ni mtu wa mshahara, wala hajali kwa ajili ya kondoo.
  14. Mimi ndimi mchungaji mwema, nawajua kondoo wangu, na walio wangu wananijua.
  15. Kama vile Baba anijuavyo mimi, nami nimjuavyo Baba; nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo.
  16. Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; hao nao imenipasa kuwaleta, na sauti yangu wataisikia; na kutakuwa na zizi moja na mchungaji mmoja.
  17. Kwa hiyo Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena.
  18. Hakuna mtu anayeninyang’anya, bali mimi nautoa kwa nafsi yangu. Ninao uwezo wa kuutoa, na ninao uwezo wa kuutwaa tena. Agizo hili nalipokea kwa Baba yangu.
  19. Kukawa tena na mafarakano kati ya Wayahudi kwa ajili ya maneno hayo.
  20. Wengi wao wakasema, Ana pepo, tena ana wazimu; mbona mnamsikia?
  21. Wengine wakasema, Maneno haya si ya mwenye pepo. Je, shetani anaweza kufungua macho ya vipofu?
  22. Na huko Yerusalemu kulikuwa na sikukuu ya kuweka wakfu, nayo ilikuwa ni majira ya baridi.
  23. Naye Yesu alikuwa akitembea Hekaluni katika ukumbi wa Sulemani.
  24. Basi Wayahudi wakamzunguka, wakamwambia, Je! utatutia shaka hata lini? Ikiwa wewe ndiwe Kristo, tuambie waziwazi.
  25. Yesu akawajibu, “Niliwaambia, lakini hamkuamini; kazi nizifanyazo kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia.”
  26. Lakini ninyi hamsadiki, kwa sababu ninyi si wa kondoo wangu, kama nilivyowaambia.
  27. Kondoo wangu waisikia sauti yangu, nami nawajua, nao wanifuata;
  28. Nami nawapa uzima wa milele; na hawataangamia kamwe, wala hakuna mtu atakayewapokonya kutoka mkononi mwangu.
  29. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya kutoka mkononi mwa Baba yangu.
  30. Mimi na Baba yangu tu umoja.
  31. Basi Wayahudi wakaokota mawe tena ili wampige.
  32. Yesu akawajibu, Kazi nyingi njema nimewaonyesha zitokazo kwa Baba; kwa ajili ya kazi ipi kati ya hizo mnanipiga kwa mawe?
  33. Wayahudi wakamjibu, Kwa ajili ya kazi njema hatukupigi mawe; bali kwa kukufuru; na kwa kuwa wewe uliye mwanadamu wajifanya kuwa Mungu.
  34. Yesu akawajibu, Je! haikuandikwa katika torati yenu, Mimi nilisema, Ninyi ni miungu?
  35. Ikiwa aliwaita miungu wale waliojiliwa na neno la Mungu, na andiko haliwezi kutanguka;
  36. Yeye ambaye Baba alimtakasa na kumtuma ulimwenguni mwasema, Unakufuru; kwa sababu nilisema, Mimi ni Mwana wa Mungu?
  37. Ikiwa sifanyi kazi za Baba yangu, msiniamini.
  38. Lakini nikizifanya, ijapokuwa hamniamini, ziaminini hizo kazi; mpate kujua na kuamini ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ndani yake.
  39. Kwa hiyo wakatafuta tena kumkamata, lakini akaponyoka mikononi mwao.
  40. Akaenda tena ng’ambo ya Yordani mpaka mahali pale Yohana alipobatiza hapo kwanza; na huko alikaa.
  41. Watu wengi wakamwendea, wakasema, Yohana hakufanya ishara yoyote;
  42. Na wengi wakamwamini huko.