Biblia ya King James Version

Ufunuo, Sura ya 22:

  1. Kisha akanionyesha mto safi wa maji ya uzima, angavu kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo.
  2. Katikati ya njia kuu yake, na upande huu wa ule mto, palikuwa na mti wa uzima, uzaao matunda ya namna kumi na mbili, unaozaa matunda yake kila mwezi; na majani ya mti huo yalikuwa ya kuponya mataifa.
  3. Wala hapatakuwa na laana tena, bali kiti cha enzi cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kitakuwa ndani yake; na watumishi wake watamtumikia;
  4. Nao watamwona uso wake; na jina lake litakuwa katika vipaji vya nyuso zao.
  5. Wala hapatakuwa na usiku huko; na hawana haja ya taa, wala mwanga wa jua; kwa kuwa Bwana Mungu huwatia nuru, nao watatawala milele na milele.
  6. Naye akaniambia, Maneno haya ni amini na kweli, na Bwana, Mungu wa manabii watakatifu, alimtuma malaika wake kuwaonyesha watumishi wake mambo ambayo hayana budi kufanyika upesi.
  7. Tazama, naja upesi; heri yeye ayashikaye maneno ya unabii wa kitabu hiki.
  8. Nami Yohana niliyaona haya na kuyasikia. Nami niliposikia na kuona, nikaanguka kifudifudi kuabudu mbele ya miguu ya yule malaika aliyenionyesha mambo haya.
  9. Kisha akaniambia, Angalia, usifanye hivi, kwa maana mimi ni mtumishi mwenzako, na wa ndugu zako manabii, na wao wayashikao maneno ya kitabu hiki;
  10. Naye akaniambia, Usiyatie muhuri maneno ya unabii wa kitabu hiki, kwa maana wakati umekaribia.
  11. Mwenye kudhulumu na azidi kudhulumu; na mwenye uchafu na azidi kuwa mchafu; na mwenye haki na azidi kufanya haki; na mtakatifu na azidi kutakaswa.
  12. Na tazama, naja upesi; na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.
  13. Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho.
  14. Heri wazishikao amri zake, wawe na amri kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake.
  15. Huko nje wako mbwa, na wachawi, na wazinzi, na wauaji, na hao waabuduo sanamu, na kila mtu apendaye uongo na kuufanya.
  16. Mimi Yesu nimemtuma malaika wangu kuwashuhudia ninyi mambo haya katika makanisa. Mimi ndimi niliye shina na mzao wa Daudi, ile nyota yenye kung’aa ya asubuhi.
  17. Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo. Na mwenye kiu na aje. Na ye yote atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.
  18. Kwa maana namshuhudia kila mtu ayasikiaye maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mtu ye yote akiyaongeza, Mungu atamwongezea hayo mapigo yaliyoandikwa katika kitabu hiki;
  19. Na mtu ye yote akiondoa katika maneno ya unabii wa kitabu hiki, Mungu atamwondolea sehemu yake katika kitabu cha uzima, na katika ule mji mtakatifu, na katika hayo yaliyoandikwa katika kitabu hiki.
  20. Yeye anayeyashuhudia haya asema, Hakika naja upesi. Amina. Hata hivyo, njoo, Bwana Yesu.
  21. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi nyote. Amina.