Biblia ya King James Version
1 Wakorintho, Sura ya 2:
- Nami, ndugu zangu, nilipokuja kwenu, sikuja kwa ufasaha wa usemi, wala wa hekima, niwahubiri ushuhuda wa Mungu.
- Kwa maana naliazimu nisijue neno lo lote kwenu ila Yesu Kristo, naye amesulubiwa.
- Nami nalikuwa kwenu katika udhaifu na woga na matetemeko mengi.
- Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kuvutia akili ya watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu.
- Ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.
- Lakini twanena hekima miongoni mwao walio wakamilifu;
- Bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele kwa utukufu wetu;
- Jambo ambalo wakuu wa dunia hii hawakulifahamu; kwa maana kama wangalilijua, wasingalimsulubisha Bwana wa utukufu.
- Lakini kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao.
- Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho wake, maana Roho huchunguza yote, naam, mafumbo ya Mungu.
- Kwa maana ni nani ajuaye mambo ya mwanadamu isipokuwa roho ya mwanadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu.
- Sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu; ili tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu.
- Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya wanadamu, bali yanayofundishwa na Roho; tukilinganisha mambo ya rohoni na ya rohoni.
- Lakini mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu, maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa sababu yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.
- Lakini mtu wa rohoni huyatambua yote, wala yeye hatambuliwi na mtu.
- Maana ni nani aliyeijua nia ya Bwana, apate kumfundisha? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo.